

Na Mwandishi Wetu WAMACHINGA
Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Mheshimiwa Albert Chalamila ameutaka uongozi wa wafanya biashara wa biashara ndogondogo eneo la Kariakoo waanze kufungua barabara magari yaweze kupita ili soko hilo litakapozinduliwa kusiwe na changamoto ya kuingia na kutoka eneo hilo.
Ametoa wito huo leo Mei 28,2025 wakati akizungumza na waadishi wa habari kuhusu maendeleo ya soko la Kariakoo katika ukumbi wa Anatoglo Jijini Dar es salaam.
Amesema kuwa wafanyabiashara wote hasa wabiashara ndogondogo wameandaliwa utaratibu maalum wa sehemu za kupanga biashara zao,hivyo ametoa muda wa wiki mbili kwa uongozi wa machinga kukaa na wafanyabiashara hao na kuwaeleza nia ya Serikali na namna ya kufungua njia ili soko liweze kuwa na tija kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa.
“Nichukue fursa hii kuwataarifu kuwa soko hili kwa sasa limefikia asilimia 98,na yamebaki mambo machache tu kukamilika kabla ya ufunguzi wake”.Alisema
RC Chalamila amesema kuwa kutokana na umuhimu mkubwa wa soko la Kariakoo Mhe.Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alielekeza Shirika la Nyumba la Taifa(NHC) kuingia ubia na wafanyabiashara ili kuweza kuongeza huduma za maduka kwa wafanyabiashara.
Amesema kuwa soko la Kariakoo ni kitovu kikubwa na alama ya biashara Tanzania hivyo tuendelee kulilinda, kuboresha, kudumisha na kulifanya kuwa safi ili kubeba na kutafsiri diplomasia kiuchumi ambayo Mhe. Rais ameendelea kuisisitiza nyakati zote.
Kwa upande wake Mtendaji wa shirika la masoko Kariakoo Ashraf Abdulkarim amesema kuwa wamejipanga kuhakikisha wanawarejesha wafanya biashara katika maeneo yao kama ilivyokuwa ameelekeza Rais Dkt Samia Suluhu Hassan.
Ikumbukwe kuwa soko hilo la Kariakoo limefanyiwa ukarabati mkubwa na kujengwa jengo lingine jipya la soko mara baada ya ajali ya moto iliyoteketeza mali za wafanyabiashara wa soko hilo.